(UTABILI) WASANII 20 WA BONGO MOVIES KUFARIKI MWEZI HUU, SOMA HAPA

Hamida Hassan na Gladness Mallya
HUKU makovu ya maumivu ya kuondokewa mfululizo na mastaa wanne wa filamu za Kibongo katika kipindi cha mwezi mmoja yakiwa hayajapona nabii naye ameibuka na kuweka wazi utabiri wake mzito kuhusu wasanii nchini hivyo kuwa sanjari na Maalim Hassan Yahya Hussein.


Maalim Hassan Yahya Hussein akiwa kwenye ofisi za Global Publishers. Hata hivyo, kabla ya kusonga mbele, tujikumbushe kwamba mastaa waliotangulia mbele ya haki kwa kufuatana ni
Adam Philip Kuambiana, Recho Leo Haule, George Otieno Owino ‘Tyson’ na Said Ngamba ‘Mzee Small’.

Kabla ya kifo cha Mzee Small, mtabiri maarufu nchini, Maalim Hassan ambaye ni mrithi wa baba yake marehemu Sheikh Hussein Yahya alitabiri kutokea vifo zaidi hadi Aprili mwakani.
Katika mahojiano, Maalim Hassan alisema mastaa wengi duniani wataendelea kuaga dunia katika kipindi hicho cha mwaka mmoja wa utabiri, lakini alitoa masharti kwa wasanii kuyazingatia ili kujikinga na vifo hivyo.


UZITO WA UTABIRI MPYA
Achana na Maalim Hassan, safari hii ameibuka Nabii wa Huduma ya Ufufuo iliyopo Buza jijini Dar es Salaam, Yaspi Paul Bendera (pichani) ambaye amekazia kuwa vifo kwa wasanii wa Kibongo vitaendelea.
Akizungumza bila hofu na gazeti hili juzu, Nabii Bendera alisema: “Nimeona kwamba, ndani ya mwezi huu (Juni) watakufa wasanii 20. Huu si utani, ni maono.”

Nabii wa Huduma ya Ufufuo iliyopo Buza jijini Dar es Salaam, Yaspi Paul Bendera. 

MASHARTI
“Hakuna masharti magumu, Mungu anawapenda wasanii, lakini ikiwa wanataka kuepukana na vifo ninavyoviona mimi, waje kanisani kwangu niwapake mafuta matakatifu.
“Wanatakiwa kumgeukia Mungu sasa, hali siyo nzuri. Nasisitiza waje niwapake mafuta matakatifu, vinginevyo wataendelea kupukutika.”


ATUMA UJUMBE
Nabii huyo aliendelea: “Kuna msanii mmoja anasali kanisani kwangu, anaitwa Herieth (Chumila). Nilimpa huu ujumbe awafikishie wenzake. Anayepuuza na apuuze lakini nawahakikishia wakimgeukia Mungu haya mabalaa hayatawakumba kamwe.”


MAMA WA BONGO MUVI SASA
Ijumaa lilisaga lami huku na huko ili kuonana na Herieth ‘Mama wa Bongo Muvi’ kwa lengo la kuthibitisha kama kweli alipewa ujumbe huo na Nabii Bendera awafikishie wenzake.
“Ni kweli nasali pale, ni kweli pia nilitumwa na Nabii Bendera nikazungumze na wasanii wenzangu kuhusiana na maono aliyooneshwa.

Marehemu George Otieno Owino ‘Tyson’ akiwa na Mboni Masimba enzi za uhai wake “Naamini utabiri wake kwa sababu nasali pale na siku aliyotabiri mambo hayo ndiyo siku aliyofariki dunia Mzee Small, nawashauri wasanii wafuate ushauri huo, waende tu kwani wakipakwa mafuta hayatawadhuru kwa lolote kwa sababu amekuwa akitabiri mambo mengi na yametokea,” alisema Mama wa Bongo Muvi.

APINGWA NA MCHUNGAJI MWENZAKE
Licha ya utabiri huo wa aina yake wa Nabii Bendera, mchungaji mmoja wa makanisa ya kiroho ambaye hakupenda jina lake litajwe gazetini kwa kuhofia malumbano alipingana na utabiri huo akisema ni gia ya kutafutia waumini.
“Hakuna kitu kama hicho. Aseme anataka kupata waumini wengi. Kama kweli yeye alioneshwa hayo maono kwa nini asiishie kuwaombea tu? Kwa nini amesema waende kanisani kwake akawapake mafuta na asiwaelekeze waende kwenye makanisa yaliyo karibu nao?
“Huyo anataka waumini, asidanganye watu. Mungu ninayemwamini anaishi ndani ya nafsi ya mtu. Kama kweli aliona hayo, dawa yake yalikuwa maombi tu, siyo kwenda kupakwa mafuta, tena na yeye mwenyewe,” alisema mchungaji huyo.


Marehemu Recho Leo Haule enzi za uhai wake. Akaongeza: “Halafu itakuwaje avione vifo na kinga yake? Hapo naona kuna kitu. Hata hivyo, ninavyojua mimi kifo ni ahadi kutoka kwa Mungu, yeye ndiye anayepanga kwa sababu anatujua vizuri watu wake.”

WASANII WANASEMAJE?
Juzi, Ijumaa liliwatafuta wasanii wa filamu za Kibongo na kuwaeleza kuhusu utabiri huo ambapo walitoa maoni yao. Wa kwanza kabisa alikuwa ni Aunt Ezekiel ambaye alisema:
“Baada ya vifo vya wenzangu nimeingiwa na hofu kubwa, namuomba Mungu atuepushie mbali hilo.”


WILLIAM MTITU
“Huyo nabii ni muongo sana, naamini vifo vyote ni mipango ya Mungu mwenyewe. Kama ni mkweli basi awataje kwa majina watakaokufa na wafe kweli na wala si kutaja tu idadi.
“Kiukweli wasanii tumechoka na hawa watabiri, tunaomba serikali itusaidie kuwachukulia hatua, wakamatwe haraka, yaani tuna uchungu mpaka basi, au kama vipi tuletewe tuwapige mangumi.”
MSANII KITALE
“Naamini binadamu kufa ni mipango ya Mungu hakuna anayeongea na Mungu, ninachoamini nabii aliyekuwepo ni Musa tu ambaye alikuwa anatabiri kitu na kikatokea.”


Marehemu Adam Philip Kuambiana,enzi za uhai wake. 

HALIMA YAHYA ‘DAVINA’
“Jamani kila kukicha wanajitokeza watabiri na manabii wengi, mimi siamini katika hilo alilolisema, wengine wanataka tu biashara zao ziende, tukifa ni mpango ya Mungu.”


SIMON MWAKIFWAMBA
“Mimi naamini, maana ufuska umezidi, kuna madai kwamba watu wanasagana, ushoga, wasanii kuzungukana wao kwa wao kama kandambili kimapenzi na ushirikina.
“Kutokana na mambo haya yote lazima Mungu atuchape fimbo, hivyo mimi nitaenda na watu wangu kwa huyo nabii kwa sababu anahubiri Neno la Mungu na siyo mganga kama wasanii wengi wanavyoabudu waganga.
“Nikienda peke yangu nitaambiwa nimesikia mwenyewe sasa nitaongozana na wasanii wengine ili tukasikie wote.”


ELIZABETH MICHAEL ‘LULU’
“Kiukweli inatisha na inaogopesha lakini mimi ninasali kwa imani yangu na siwezi kusema utabiri hamna au upo kwani hata kwenye Biblia upo ila siwezi kujua huyu anasema kweli au uongo kwa sababu nabii hana alama.”


Marehemu Said Ngamba ‘Mzee Small’ enzi za uhai wake. AISHA BUI
“Mimi ninachoamini hakuna binadamu anayejua kesho kitatokea nini, kama yeye mtabiri kweli basi na yeye ajitabirie atakufa lini.”


SABRINA RUPIA ‘CATHY’
“Mimi namwamini Mungu, pia kila msanii aliyekufa ni ahadi ya Mungu, nikifa leo naamini Mungu amenipenda na watu wasiwe na wasiwasi na kifo changu.
“Huyo nabii ni nani mpaka ajue tutakufa? Hakuna kitu kama hicho, mimi siamini kabisa. Kikubwa wasanii tunatakiwa tumwombe Mungu kwani ndiyo kila kitu.”


MTAZAMO
Mtazamo wa gazeti hili si kuwapa hofu wasanii bali kupeleka ujumbe kwamba Mungu ni kila kitu na si vinginevyo. Binadanu wote, wakiwemo wasanii, wanatikiwa kusali kwa imani zao ili maisha yaendelee bila kusikiliza mbiu kutoka kwa watu wengine.CREDIT: GPL