Mwanaume aharibu mali zote za mpenzi wake baada ya kunyimwa tendo la ndoa



RB nambari TBT/RB/3478/2014  ya Kituo cha Polisi Tabata, jijini Dar es Salaam ina kesi ya dereva taksi aliyepatikana kwa jina moja la Lindoya akidaiwa kuharibu mali za Asia Hakika kwa sababu eti alinyimwa unyumba.
 
Asia Hakika anayedai kuharibiwa mali zake na dereva taksi aitwaye Lindoya.
Mlalamikaji Asia, mkazi wa Tabata – Chama na mtuhumiwa Lindoya mwenye makazi yake Mbezi – Makabe ni wapenzi wa muda mrefu sasa, lakini baada ya Asia kugundua kuwa mwenzake ana mke na watoto, akagoma kumpa tendo la ndoa, jambo lililoibua kisanga hicho.
 
Akizungumza na Uwazi, Asia alisema: “Lindoya ni mpenzi wangu, tulikuwa tunaelekea kuwa mume na mke, maana tumeishi kwa miaka miwili sasa, lakini siku zote amenieleza kuwa hana mke wala watoto, lakini nimegundua kuwa alinidanganya.

“Ana mke na watoto wawili, nikaamua nimuache aendelee na familia yake. Akakataa, anataka kunitumia tu. Nilipomkatalia ndiyo akaamua kuniharibia vitu vyangu.  Alinikuta nina vitu vya ndani nilivyonunua kwa fedha zangu,  nimepanga chumba kwa pesa yangu na aliniomba tuishi pamoja nikamkubalia.
 
“Baadaye akaanza kujenga nyumba huko Mbezi ya Makabe, nilifurahi sana niliamini kuwa tukioana tutakua tunaishi huko lakini cha kushangaza baada ya kumaliza kujenga alimfuata mkewe huko Mbeya, wakahamia na watoto wake.”
 
Alisema, mpenzi wake huyo zilipendwa, alimwambia asikanyage nyumbani kwake kwa kuwa mkewe amekuja, jambo ambalo alikubaliana nalo kwa sharti kuwa wasitishe uhusiano wao lakini Lindoya akaonekana kutoridhika.
 
Baadhi ya mali za Asia Hakika zilizoharibiwa.
“Siku moja nikiwa kazini, alifika nyumbani kwangu akafungua mlango kwa funguo wake, maana kila mmoja alikuwa na wake; akaharibu mali zote ndani, akaacha kitanda tu. Nimeumia sana kwa kweli,” alisema Asia.
 
Kwa sasa kesi hiyo ipo katika Kituo cha Polisi Tabata kwa uchunguzi ambapo jalada la uchunguzi limeandikishwa kwa namba TBT/IR/2032/2014.

Chanzo: Uwazi/GPL