Mwanamke Aliyemng'ata Hausigeli na kumchoma Pasi Aachiwa


Mtuhumiwa wa kesi ya kujeruhi kwa kumng'ata sehemu mbalimbali za mwili  mfanyakazi wa ndani, inayomkabili Amina Maige (42) amepatiwa dhamana jana baada  ya mahakama kuthibitisha kuwa hasira kutoka kwa wananchi zimepungua.
 
Hakimu wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kinondoni, Yohana Yongolo alisema ameridhishwa na ufafanuzi uliotolewa na Mwendesha mashitaka wa Serikali pamoja na Wakili wa mshitakiwa kuwa haki ya dhamana itolewe kwa kufuata masharti na kwamba hakuna uhalifu wowote utakaofanyika dhidi ya mshitakiwa huyo.
 
Hakimu  Yongolo alitoa masharti ya dhamana ambayo yalimtaka Maige kutoondoka nje ya Dar es salaam bila ya ruhusa ya mahakama hiyo.
 
Pia alitoa masharti ya kuwa na wadhamini wawili wa kuaminiwa kutoka taasisi inayotambulika hapa nchini ambapo mdhamini huyo anaweza kuwa mwajiriwa, mfanya biashara na mkulima.
 
Alisema wadhamini hao watatakiwa kusaini hati ya makubaliano kwa kila mmoja kulipa Sh milioni tatu.
 
Aliongeza kuwa kesi hiyo itasikilizwa Julai 22 mwaka huu.
 
Maige alidaiwa Januari mwaka jana hadi Juni mwaka huu, alimng'ata na kumchoma na  pasi  sehemu mbalimbali za mwili wa  mfanyakazi waje wa ndani Yusta Kashinde (20) na kumsababishia maumivu mwilini.